Home | Terms & Conditions | Help

May 18, 2024, 8:30 pm

NEWS: RIPOTI YA AJALI YA NDEGE YA PRECISION YABAINI UZEMBA WA UONGOZI

Dar es Salaam. Ripoti ya awali ya uchunguzi wa ajali ya ndege ya Shirika la Precision Air, imebaini udhaifu mkubwa katika uongozi hasa ikitupia jicho katika Jeshi la wanamaji baada ya ripoti kufafanua kuwa Jeshi la Polisi Kitengo cha Wanamaji kilipewa taarifa dakika 15 baada ya tukio lakini hakikufika kwa wakati.

Ajali ya ndege ya Precision ilitokea siku ya Jumapili ya Novemba 6, 2022 ilikuwa na watu 43 kati yao, 39 walikuwa abiria, marubani wawili na wahudumu wawili. katika ajali hyo watu 19 walifariki dunia na 24 kuokolewa.

Kulingana na ripoti hiyo, iliyotolewa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, jana Jumatatu Novemba 22, 2022 askari hao wenye boti 400 HP inayotumika kwa shughuli za doria na uokozi, walishindwa kuitumia wakati huo kwa kuwa haikuwa bandarini.

Hata hivyo, inaeleza askari walishindwa kupiga mbizi kutokana na mitungi waliyokuwa nayo kukosa gesi.

“Boti ilikuwa mbali kwa majukumu ya doria. Ilifika eneo la tukio saa 13:49 mchana, hata hivyo askari walishindwa kupiga mbizi kwa kuwa vifaa vyao vya oksijeni vilikosa hewa hiyo,” imeandikwa katika ripoti hiyo.

Kulingana na ripoti hiyo, hali ya hewa ya uwanja wa ndege wa Bukoba ilikuwa shwari wakati ndege inaanza safari, lakini ilibadilika ghafla kuanzia

“Hali ya hewa ilikuwa nzuri hadi saa 08:20 asubuhi, ilibadilika ghafla, mvua ikaanza kunyesha na ngurumo, mawingu mazito na upepo mkali,” ilieleza taarifa hiyo.

Hata hivyo, uchunguzi wa mabaki, umeonyesha ilikuwaa vigumu kufungua mlango wa nyumba wa abiria wa ndege hiyo kwa kuwa tayari ulikuwa umezama ndani ya maji.

“Ndege hiyo ilitua majini (Ziwa Victoria) umbali wa mita 500 kutoka njia ya kurukia ndege. Kina cha maji katika eneo hilo kilikuwa mita 5.4,” alisema.

Aidha, waliofariki wengi wao walikuwa siti za mbele na kati ambao hawakuweza kufungua mikanda kwa haraka.

Kuharibika sehemu ya chini ya ndege kuliruhusu maji mengi kuingia ndani kwa msukumo mkubwa na kuwafunika kwa mujibu wa ripoti hiyo.

"Mhudumu mmoja ndiye aliyefungua mlango wa kushoto wa abiria, alisaidiwa na abiria kuusukuma. Baadhi ya manusura akiwemo mtoto mwenye miezi 18 na mama yake waliokolewa kwa njia hiyo.

"Wavuvi walikuja dakika tano baadaye na waliwapakia manusura katika boti yao, kwa hiyo abiria 24 wakiwemo wahudumu wawili walipona," imeeleza taarifa hiyo .