Home | Terms & Conditions | Help

May 18, 2024, 10:29 pm

NEWS: SABABU ZA WAZIRI MKUU WA UINGEREZA LIZ TRUSS KUJIUZULU

Waziri mkuu wa Uingereza Liz Truss amejiuzulu. Truss amejiuzulu hii leo, wiki sita tu baada ya kuchukuwa wadhifa huo, licha ya hapo jana kusisitiza kwamba hatang'atuka mamlakani.

Truss amejiuzulu baada ya kusambaratika kwa mpango wake wa makato ya kodi na kupoteza uungwaji mkono wa wabunge wengi wa chama chake tawala cha Conservative. Katika hotuba ya kujiuzulu kwake, Truss amesema kuwa alichukuwa madaraka wakati wa msukomsuko wa kiuchumi nchini Uingereza na kimataifa, huku familia nyingi na wafanyabiashara wakiwa na wasiwasi juu ya mzigo mkubwa wa madeni.
Truss ameongeza kusema kwamba anatambua kwamba kutokana na hali ilivyo, hawezi kutimiza jukumu aliyopewa na chama cha Conservative.Kujiuzulu kwa Truss kunakiacha chama cha Conservative kilichogawanyika. Wakati huo huo, aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo Boris Johnson anatarajiwa kujitosa katika kinyang'anyiro cha uongozi wa chama cha Conservative ili kujaza nafasi ya Liz Truss aliyejiuzulu.

Haya yameripotiwa na gazeti la The Times. Katika ujumbe katika mtandao wa twitter, mhariri wa gazeti hilo la times Steven Swinford, amesema Boris anasikiliza ushauri kutoka kwa watu wake wa karibu lakini anaamini ni suala la maslahi ya taifa.